Bukobawadau

RIDHIWANI KIKWETE AANIKA UTAJIRI WAKE


*Aeleza adha za kuwa mtoto wa Rais, ataja fedha alizonazo benki
*Azungumzia urais 2015, uhusiano wake na Membe, Lowassa
*Achambua mgogoro wake na Hussein Bashe, Dk. Wilbrod Slaa
Mtoto wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwani Kikwete, amefanya mahojiano maalum na Gazeti la JAMHURI nyumbani kwake Mikocheni jijini Dar es Salaam, Machi 30, mwaka huu, na kuzungumzia masuala mbalimbali yanayomhusu yeye binafsi na mengine yanayolihusu Taifa.
Miongoni mwa mambo aliyoyazungumzia kwa kina ni utajiri wake hasa kutokana na kutajwa kuwa ana ukwasi wa kutisha, hekaheka za urais, na anavyowafahamu Waziri Mkuu (mstaafu), Edward Lowassa, na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.

Pia amezungumzia ugomvi wake na Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Hussein Bashe.

JAMHURI: Kuna taarifa kuwa wewe ni tajiri mkubwa hapa nchini na umepata utajiri usioelezeka ndani ya muda mfupi. Ukweli ukoje?

RIDHIWANI: Maneno haya nimeyasikia kila kona. Nimesingiziwa ninamiliki mali nyingi ajabu. Kila kampuni inayoanzishwa naambiwa ni yangu. Kila jengo kubwa na refu hapa nchini wanasema ni la Ridhiwani. Na sasa nadhani kimebaki kitu kimoja -  kunikabidhi wake za watu - maana nchi hii kila kampuni naambiwa ya kwangu. Kila kitu, jamaani!

Pamoja na maneno mengi sana, sitetereki kwa sababu moja kubwa ni kwamba niliandaliwa kukabiliana na hali hii. Wakati mzee wangu anaingia kwenye siasa (kuwania urais) nilikutana na Abdallah Mwinyi (mtoto wa rais mtaafu mzee Mwinyi), akaniambia changamoto nitakazokutana nazo kama mtoto wa rais, na sasa nazishuhudia vilivyo.

Hivi sasa nasingiziwa kampuni ya ASAS (ya Iringa). Mwenye ASAS namfahamu, watoto wake akina Salim Abri nawafahamu na nilikutana nao nikiwa Iringa shuleni. Nilipofuatilia historia ya kampuni yao, kampuni ile ilianzishwa mwaka 1939. Miaka hiyo hakukuwapo na wazo la mimi kuzaliwa.

Nilipoenda eneo la Ipogolo nikakuta kuna petrol station ya ASAS, sasa cha kushangaza, watu wanasema mimi nahusika kwenye ile kampuni. Nashindwa kuelewa mimi nahusikaje? Ila kibaya zaidi ukisema, kwenye memorandum za kampuni ninazosingiziwa kumiliki huwezi kukuta Ridhiwani ni sehemu ya umiliki. Watanzania wamejenga utamaduni wa kusema sana, siyo ASAS peke yake, wanasema kila kampuni ni yangu hapa nchini. Kila jengo refu wanasema ni langu. Mimi nasema sina biashara hizo. Labda baadaye Mungu akipenda.

Lakini ifahamike kuwa kufanya biashara si dhambi. Dhambi ni kufanya biashara ukawa na mali zisizoelezeka chimbuko lake. Kwa mfano, ipo siku nilisikia habari eti Mzee [Reginald] Mengi anadaiwa benki. Nikasema hawa wa ajabu kweli. Wanadhani huyu ana mwembe wa kupukutisha fedha, mfanyabiashara lazima akope na alipe. Kudaiwa benki si tatizo.
Njia mojawapo ni kuweza kuona opportunity (fursa) nzuri ambazo hazina migogoro ukafanikisha na kupatiwa kipato. Mojawapo ni hiyo kukopa fedha benki au kukopa kwa watu binafsi. Lakini wanaposema Ridhiwani ana hili, tuulizane, je ni kweli anavyo hivi vitu? Hizi ni fitina tu.

Kinachonisikitisha, wa siasa wanasikia mambo haya, wanayabeba na kuyachukua kwenye majukwaa ya kisiasa. Kipindi fulani Bwana [Dr. Wilbrod] Slaa akaenda kwenye mikutano akasema nina utajiri wa kutisha. Anataja kuwa nina magari mengi mno, ukimuuliza gari aina gani namiliki, hata rangi hajui.

Nimempeleka mahakamani na hivi karibuni hukumu itatolewa. Hatuwezi kumwachia. Mimi siwezi kumpiga ngumu - ni mzee wangu namheshimu sana. Sehemu pekee inayoweza kunipatia haki yangu ni mahakama, ndiyo maana nimepeleka kesi mahakamani.

JAMHURI: Unasema unasingiziwa kumiliki mali. Hebu wewe eleza unamiliki nini?
RIDHIWANI: Mimi namiliki gari moja, nyumba moja, na hii nyumba nimepewa na Mzee [Rais Kikwete]. Nina viwanja viwili Bagamoyo, shamba jingine liko Chalinze na na jingine Lugoba, basi. Sijawahi kutamani kufanya biashara ya mafuta, sina kiwanda, labda kampuni yangu ya sheria – GRK. Familia haina kiwanda cha mifuko ya karatasi. Sisi tunalima mananasi tunauza.

JAMHURI: Kwa nini usingiziwe?

RIDHIWANI: Hii ni hulka tu imeibuka hapa nchini. Kwa hapa Dar es Salaam kitu pekee kilichobaki ni kukabidhiwa wake za watu. Mimi siwezi kufanya kitu chochote bila kumshirikisha mzee wangu. Hata kwenye kampuni yetu, tunapopata biashara kubwa siikubali hivi hivi. Maana najiuliza mtu asije kwa sababu Ridhiwani ni mwanasheria, akatumia jina langu, la mzee (Rais Kikwete). Hilo hatulifanyi.

JAMHURI: Hivi karibuni zilisambaa taarifa kuwa ulikamatwa nchini China ukiwa na dawa za kulevya. Likoje hili?
RIDHIWANI: Mimi siwezi kujisemea, rekodi zangu zipo airport. Sijawahi kufika China, India, Israel, wala Palestina. Kwa Mashariki ya Mbali na Mashariki ya Kati nchi pekee niliyokwenda ni Dubai tu. Tarehe inayosemwa kuwa nilikamatwa China, ilikuwa ni siku ya Uhuru wa Burundi au Rwanda. Siku hiyo mzee [Kikwete] alikuwa in one of those countries (katika moja ya nchi hizo).

Kwamba mimi nilikuwa nimekamatwa China na mzee wangu akaitwa, ni upuuzi mtupu. Kwanza China si safari ya nusu saa, ni safari ya zaidi ya siku mbili. Sasa wamechonga habari hii eti mzee akaenda kunikomboa China nikiwa nimeshikiliwa… Yote haya ni kampeni za kujaribu kuchafua jina langu. Sijawahi kufanya biashara hiyo [ya dawa za kulevya], na siweza kufanya hivyo.

JAMHURI: Katika kusingiziwa huko, ni lipi ulilosingizwa ambalo likakukera sana?

RIDHIWANI: Katika maisha yangu nilikerwa sana na stori iliyochapishwa na gazeti [jina linahifadhiwa] eti mimi nashiriki kwenye mpango wa kumpindua baba yangu. Hili liliniuma na kunikera sana. Yaani mimi nishiriki mpango wa kumpindua baba? Du, hii ni hatari.

JAMHURI: Ukiacha hizo mali unazosema unasingizwa, hivi kwenye akaunti wewe una fedha kiasi gani cha fedha kwa sasa?
RIDHIWANI: Sina cha kuficha, na mimi sijapiga hesabu kwenye akaunti zangu kujua kuna kiasi gani, lakini siHiHidhani kama ninaweza kuzidi shilingi milioni 20.
Kuwa mtoto wa Rais
JAMHURI: Hivi maisha ya kuwa mtoto wa Rais yakoje?

RIDHIWANI: Ni maisha magumu sana. Mimi nadhani Rais ajaye ni vyema asiwe na watoto. Labda wawe kama mapapa. Unakuwa kardinali halafu ndiyo uwe Rais. Ukiangalia jinsi watu wanavyojaribu ku-portray (kuonesha) picha ya mtu, ni tofauti.

Baba ni mtu ambaye hana tamaa ya mali. Ni mtu anayeweza kufanikisha miradi ya mabilioni, lakini asitamani kuwa na senti tano. Ila nikiangalia jinsi watu wanavyomsema, mpaka mimi najiuliza kuwa huyu ndiye mzee wangu ninayemjua?

Yeye anasema ‘sina tamaa ya mali. Nina nyumba, shamba langu la Msoga, ng’ombe wangu, na nikistaafu wataendelea kunipa ulinzi na kunilipa pensheni, inatosha.’ Sisi hatuko huru hivyo. Watu wanakunyooshea vidole, wanasema huyu kafanya hivi, mara vile hadi inachosha. Juzi nimekwenda kwenye maziko Arusha, nimekutana na mtu akanisalimia kisha akaniuliza, ‘Ridhiwani ndiyo wewe? Nimeambiwa una fedha nyingi sana.’

Mimi nasema inawezekana watu hawanifahamu maisha yangu niliyozaliwa nayo, niliyokua nayo. Jamii ya Watanzania inalishwa maneno, hata kama jambo hujalifanya wanasema ama anatufanyia sinema, au anatulaghai. Nchi hii kwa sasa kila mtu ana tafsiri yake kwa kila jambo.

JAMHURI: Kwenye siasa. Mnaichukuliaje hali ya familia moja kuwa na wajumbe watatu wa NEC?

RIDHIWANI: Maisha ya familia kuwa na wajumbe watatu wa NEC - kuna ya familia yangu na ya Bagamoyo. Mimi nashughulika na ya Bagamoyo, Mama Salma na watu wake wa Lindi, Jakaya siasa yake na Watanzania.

Mimi siangalii kuwa na wajumbe watatu wa NEC ndani ya nyumba, ninachoangalia ni nini tunalifanyia Taifa katika utumishi wetu. Mimi eneo langu ni Bagamoyo. Ninalolifanya mimi halina uhusiano wowote na Jakaya Kikwete, tunashauriana vizuri, tunafanya kazi kwa pamoja, tusingependa Watanzania watuchukie kwa kushindwa kuwatumikia.

JAMHURI: Unauonaje mwelekeo wa siasa nchini?

RIDHIWANI: Mwelekeo wa siasa, kulikuwa na dalili mbaya. Mauaji ya viongozi wa dini, mauaji ya wanaharakati. Tumeshuhudia watu wanateswa. Ukitafuta chanzo ni nini, chanzo ni kwa baadhi ya watu kufikia malengo. Yule mtuhumiwa mmojawapo wa mauaji ya Padri [Evarist] amekamatwa. Uchunguzi ambao unaendelea juu ya involvement [uhusika] ya viongozi juu ya mauaji na mateso dhidi ya waandishi wa habari ni muhimu.

Vyombo vya ulinzi na usalama lazima sasa viamke. Tusisubiri matukio ndiyo yatuongoze kufanya kazi. Mauaji kwa mfano ya Padri wa Zanzibar, kuteswa kwa Kibanda, Ulimboka au mauaji ya Chacha Wangwe, hayakutokea kwa bahati mbaya. Inaonesha upo mkakati wa baadhi ya watu. Hatuwezi kuwanyooshea kidole Chadema au wanaotaka urais, watu wanataka kutengeneza picha ili baadaye wapate advantage (faida).

Ikitokea kuwa Lwakatare ameshiriki mkakati wa kutesa waandishi wa habari ambao wanaonekana ni anti-Chadema (wanaoipinga Chadema), sisi wengine tuliopo ndani ya CCM itakuwaje? Vyombo vya dola wanapaswa wawe wepesi kutenda ili yanapotokea iwe rahisi kudhibiti hali.

Mimi naamini ile video ya Bwana Lwakatare, ile video ukiiangalia, sitaki kuamini kwamba ilirushwa kwenye mtandao wa vyombo vya dola ndipo vilianza kuifanyia kazi. Vyombo vya dola vichunguze zaidi huyu mtu anazungumzia mauaji ya Morogoro, mauaji ya Iringa, itafutwe maana huenda naye aliyefanya alilipwa hela akafanya hivyo.
Lazima uwepo uchunguzi wa kina. Haiwezi kuwa Serikali iliyoapa kulinda maisha ya watu ghafla igeuke kuua wananchi. Mimi hili nasema hapana. Vyombo vya dola vijipenyeze kila mahali viwe na taarifa za uhakika kwa wakati na kuzifanyia kazi.
Uhusiano wake na Membe
JAMHURI: Wewe na Waziri Membe mna uhusiano gani?

RIDHIWANI: Kwanza niseme uhusiano wangu, siasa yangu si ya Jakaya, si ya Mama Salma, Jakaya ana nafasi mbili kwangu. Kwanza ana nafasi ya baba na nafasi ya Mwenyekiti wa chama. Namheshimu kama baba, kama Mwenyekiti.

Membe mimi ni rafiki yangu, lakini pia Membe ni baba yangu, mentor (mlezi) wangu. Namwangalia kama mtu unayeweza ukamwiga kwa mawazo yake na utendaji wake. Nimemfahamu mara ya kwanza mwaka 1986. Tulikuwa tumetoka Arusha tumekuja Dar es Salaam na baba. Tukaenda nyumbani kwake Membe, tukaenda wote. Wakawa wanazungumza. Ni marafiki wa siku nyingi. Tukiwa Nachingwea alikuwa anafika kumsabahi baba. Kulikuwapo na ndege inatua pale Nachingwea kila akitoka airport anapitia kwetu.

JAMHURI: Ziliripotiwa taarifa kwenye uchaguzi wa NEC Dodoma kuwa wewe na familia nzima mlikuwa mnampigia kampeni Membe. Unalizungumziaje hili?

RIDHIWANI: Mtu ambaye siku zote unajua ni mzuri, unakunywa chai kwake, una jambo anakusaidia, then ile attachment (ule mshikamano), sasa imefika sehemu Membe anataka jambo, najikuta nalazimika kumsaidia. Sipendi kuona Chama Cha Mapinduzi kinampoteza mtu mzuri kama Membe eti kwa sababu ya uchaguzi wa 2015. Historia ya Maisha ya Membe, watu wanapaswa waijue. Historia yake, Membe ametokea wapi? Watu wamjue vizuri, kwa sababu nahisi watu hawamjui.

Suala la mtu kuwa Rais wa Tanzania si suala ambalo mimi Ridhiwani naweza kuamua. Wenye kuamua ni wanachi wasiokuwa na maji ya kunywa, wasio na uhakika wa soko, wenye shida ya njaa, hawa ndiyo wanaotaka Rais, si Ridhiwani na wala si haya makundi yanayosema.

Mimi binafsi jambo hili sikuweza kulivumilia, niliwatafuta marafiki zangu nikasema tumsaidie huyu (Membe). Hili halikuwa la Ridhiwani, nia ni kukisaidia chama. Kina January, kina Wassira hawakuombewa kura? Hili ni tatizo, imefika sehemu haki ya kiongozi ndani ya chama hiki inataka kupotezwa? Ni kweli mimi binafsi nilimsaidia. Mama Salma na Membe wao wote wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Lindi, sasa kama walisaidiana mimi sijui, ila fikiria mwenyewe.

JAMHURI: Watu wanasema hilo linajikita zaidi katika kumpigia debe Membe awe Rais. Je, unaridhika na sifa alizonazo?

RIDHIWANI: Ukiniuliza mimi kama mimi, I think he deserves (nafikiri ndiyo anafaa). Kwa sifa alizonazo nadhani anafaa.

Lowassa na familia ya Kikwete
JAMHURI: Kwa siku kadhaa sasa inasemwa kuwa Mheshimiwa Kikwete na Lowassa wana mgogoro. Je, wewe kama mtoto ndani ya familia unadhani hawa watu bado ni marafiki?

RIDHIWANI: Nisingependa sana kujadili mahusiano ya mzee wangu na watu wengine. Ila ninachojua mahusiano yao yalikuwa sana ni ya kikazi, si ya kifamilia. Sina kumbukumbu mimi kama mtoto kuona Bwana Lowassa akishiriki shughuli za kifamilia, wala sisi kwenda kushiriki shughuli za familia ya Lowassa.

Naweza nikawa namjua mzee wangu kuliko mtu yeyote. Mzee wangu hana kinyongo na mtu yeyote. Anasema ya kwake, na Lowassa akiomba appointment anakubaliwa anakuja Ikulu wanazungumza, anasaidiwa katika mambo yake, ila naliona tatizo kwa upande wa mashabiki wa kisiasa.

Hili lipo, ukikaa vijiweni unasikia watu wanavyomsema sana Lowassa, lakini ukiyasikia yote haya unaambiwa Lowassa amebanwa, unajiuliza aliyebanwa anakuwa namna hii? Wakati mwingine anasema mambo mengine ambayo kama binadamu yanakuudhi. Anakwenda makanisani anaendesha harambee.

Mimi nasema wanaotaka Rais wao si Bwana Jakaya Kikwete, wanaotaka Rais wao ni Watanzania. Kama wanataka Lowassa watamchagua, kama wanamtaka Membe watamchagua, kama wanamtaka [John] Magufuli watamchagua na hata kama wanakutaka wewe Manyerere watakuchagua.

JAMHURI: Hivi huko kwenye duru zako unasikia kina nani wanatajwatajwa kuwa wanaweza kugombea urais?

RIDHIWANI: Wanatajwa wengi akina Sumaye (Frederick), [Emmanuel] Nchimbi, Mathayo David, Profesa Anna Tibaijuka, Asha-Rose Migiro, na wengine wengi tu.

CCM siku zote ni chama ambacho kinaangalia Watanzania wanataka nini. Lazima tujue kwamba mgombea anayepitishwa na Chama Cha Mapinduzi, awe na sura ya kuuzika kwa wananchi. Si mgombea ambaye atakwenda halafu kesho tuwe na masikitiko. Wahusika  hawatafanya kosa hili. Lakini awe ni mtu anayeweza kusikiliza matatizo yao. CCM hawawezi kuwa wajinga kupeleka jitu ambalo litajiangalia lenyewe. Suala si mwanamke au mwanaume, bali mgombea anayeweza kukabiliana na changamoto hizi.

Misingi ya uchumi ni economic diplomacy (diplomasia ya uchumi), leo hii unakuwa na Rais ambaye mataifa yote duniani yana imani nawe. Amekuja hapa Rais wa China wa kwanza [Hu Jintao], amekuja Rais wa China mwingine [Xi Jinping], amekuja George Bush wa Marekani, Tanzania inaangaliwa vipi na dunia?

Pia ipo misingi ya nchi, ambayo mtu anaweza kuichukua nchi hii kuisogeza mbele. Jambo ambalo tusingependa litokee ni hilo. Wagombea wote wanaotajwa, wote wana sifa. Wengi wao wana sifa ambazo zinatosha kabisa kuwapeleka wawe wawakilishi wa nchi hii.
JAMHURI: Vyombo vya habari vimekukariri ukisema Rais ajaye hawezi kutoka kaskazini. Ulimaanisha nini?

RIDHIWANI: Kauli hiyo haikutoka kwangu. Ilitolewa na vijana wa Mkoa wa Pwani.
Nilihudhuria kikao hicho, lakini sikuzungumza kwenye kikao hicho. Kwenye vikao, kuna mawazo mbalimbali. Mawazo yanapotolewa ni jukumu la wale wanaosikiliza, kulichukua au kuliacha, katika kikao kile yalizungumzwa mambo mengi sana, lakini likachukuliwa hilo tu.

Kikao kile kiliitishwa kutoa onyo kwa viongozi kutokuwa wasemaji ovyo. Kauli mbaya iliyotolewa na Bwana [Frederick] Sumaye Waziri Mkuu mstaafu ilikera. Anasema eti chama kiwajibu Watanzania kuhusu maswali ya Chadema, tukasema hapana.

Sumaye wakati huo alikuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu mstaafu. Yeye ana uwezo wa kumwita Katibu Mkuu wa Chama nyumbani kwake akamweleza yanayomkera au akatumia vikao halali. Hatukuona sababu ya yeye kuwaita waandishi wa habari kuzungumzia hili. Tukaona hili jambo hakuwa sahihi. Tukaona bora tuwatake viongozi wetu wazungumze kwenye vikao halali.

Ugomvi wa Ridhiwani na Bashe
JAMHURI: Hivi ugomvi wako na Hussein Bashe unatokana na nini?
RIDHIWANI: Basically (kimsingi), sisi hatuna msuguano, ila ni uwezo wa watu kutafuta jinsi ya kutugombanisha ili wafaidike. Mimi sikumjua Bashe hadi uchaguzi wa mwaka 2007. Bashe alikuwa anagombea na mtu anaitwa Benno Malisa. Benno alikuwa rafiki yangu kwa miaka 16 hivi – nilimfahamu nikiwa form two, damu zetu zikapendana.

Benno alianza anasoma Political Science, baadaye akaja Sheria, nilipochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kitivo cha Sheria nilimteua Benno Malisa kuwa Katibu wangu. Alionesha uwezo mkubwa sana wa kutenda kazi zake. Tumeendelea hivyo mpaka 2007 Benno akajitokeza kugombea uenyekiti.

Kamati Kuu ikaamua vijana wa Bara wagombee nafasi ya Makamu Mwenyekiti, na yakarejeshwa majina matatu - Benno Malisa, Hussein Bashe na Zainabu Kawawa. Kwangu ulikuwa mtihani mkubwa. Zainabu Kawawa historia ya Mzee Kawawa na Baba yetu. Kwangu mimi ulikuwa mtihani mkubwa, lakini si kwa Bashe maana sikuwahi kukutana naye hata siku moja kabla ya 2007.

Wakati Benno anataka kugombea ile nafasi ni mmoja wa watu walionifuata, nikamwambia umeishi ndani ya Umoja wa Vijana ukiwa kiongozi. Alichaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza, baadaye akawa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana. Nikamwambia mimi kama rafiki yako nisingependa nikurudishe nyuma. Niliridhika kutokana na sifa alizokuwa nazo, nikamwambia gombea nitakuunga mkono.

Ni kweli Bashe tulikutana pale Millennium Towers, nilimwambia kuwa ‘kama Benno anagombea, sitakuunga mkono’. Niliamini na niliona amenielewa.
Majibu ya Bashe
JAMHURI imewasiliana na Bashe kuhusu kauli hii ya Ridhiwani naye amesema hivi: “Aliyefanya nimfahamu Ridhiwani ni Benno Malisa wakati tunagombea NEC pamoja mimi na Benno mwaka 2007. Mimi na Ridhiwani hatujawahi kuwa marafiki wala hatujawahi kuwa maadui. Amekuwa Mjumbe wa Baraza kwa miaka minne tukiwa wote. Suala kwamba tulitofautiana kwenye uchaguzi wa NEC mwaka jana, hiyo ni demokrasia.

Mimi nilikwenda Dodoma na kusema Membe asichaguliwe, huo ulikuwa utashi wangu wa kisiasa, kama ambavyo Ridhiwani kwenye Uchaguzi wa UVCCM, alimuunga mkono mtu mwingine, mimi nilimpinga Membe wazi.
CHANZO GAZETI JAMHURI

Next Post Previous Post
Bukobawadau